TASAC yashiriki mjadala wa kitaalamu kuhusu namna nchi ilivyojiandaa kuendana na uvumbuzi wa teknolojia mpya ya akili ya bandia (Artificial Intelligence-Al)
Kaimu Meneja wa Usajili na Ukaguzi wa Meli, Mha. Said Kaheneko wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) ameshiriki katika jopo la mjadala wa kitaalamu kuhusu namna ambavyo nchi imejiandaa kuendana na uvumbuzi wa teknolojia mpya ya akili bandia (Artificial Intelligence - AI). Mjadala huo umefanyika katika Mkutano wa 16 wa wadau wa Sekta ya Uchukuzi unaofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa Arusha (Arusha International Conference Centre-AICC) tarehe 07 Disemba, 2023.
Mha. Kaheneko amefafanua kuwa TASAC ikiwa ni mdhibiti wa usafiri kwa njia ya maji imeweka mikakati thabiti ya namna ya kukabiliana na teknolojia hiyo mpya katika vyombo vya usafiri majini. Mikakati hiyo itatekelezwa kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali ikiwa ni pamoja na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Chuo cha Usafirishaji Tanzania (NIT), Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) ambazo zina mchango katika kuendeleza na kusimamia teknolojia hii mpya.