MAKAMU MKUU WA CHUO CHA BAHARI DAR ES SALAAM (DMI) AFUNGUA WARSHA KATIKA MAADHIMISHO YA SIKU YA MABAHARIA DUNIANI
Makamu Mkuu wa Chuo cha Bahari Dar es salaam (DMI), Dkt. Wilfred Johnson amesisitiza mabaharia kuzingatia usalama wa vyombo vya usafiri majini nyakati zote wanapoendesha vyombo hivyo ili kuokoa maisha ya Watanzania. Amesema hayo akiwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa warsha ya siku moja iliyofanyika katika ukumbi wa Sk Twins Park uliopo mjini Bagamoyo.
Dkt. Wilfred amesema "Jitihada zinazofanywa kuzuia ajali za barabarani, zielekezwe pia kwenye usafiri wa majini kuzuia baadhi ya ajali zinazosababisha na makosa ya kibinadamu".
Warsha hiyo imewakusanya mabaharia, wataalam, wavuvi na viongozi mbalimbali na kujadili masuala ya namna ya kusoma ubaharia, usalama na mfumo wa kielectroniki.
Aidha, mwazilishaji wa mada ya mfumo wa kielektroniki Bw. Ally Diwani Afisa Ukaguzi na Usajili wa Meli kutoka TASAC, amesema TASAC imejipanga kuja na mfumo mpya wa kuwasajili mabaharia kielektroniki na kuwa na cheti kimoja tu chenye taarifa zote muhimu kitakachokuwa kinatambulika duniani. Hali hiyo itasaidia kuwa na takwimu sahihi za mabaharia nchini.
Hata hivyo, wakati wa mjadala wengi wa washiriki wamesema elimu bado inahitajika juu ya namna ya kutumia mfumo huo kabla kuanza kutumika rasmi.